moja

Responsive Advertisement

Na Veronica Mrema 

Si jambo la kukalia kimya tena. Ni mada muhimu, ya lazima na mahususi ambayo inapaswa mno kuzungumzwa wazi-wazi.

Afya ya akili si jambo la kulipa kisogo ndani ya jamii. Sasa, vijana wanaamua kuiweka mezani kama agenda ya wazi kwa hoja madhubuti na mjadala unaohitaji majibu.

Swali la msingi ni wapi tulipotoka, tulipo sasa, na tunapoelekea? Visa na mikasa vimetawala miaka ya karibuni mashuleni, ambavyo vinahusishwa moja kwa moja na changamoto za akili.

Ndani ya vyuo mbalimbali imeripotiwa wanafunzi kadhaa kujizuru mathalani kujitoa uhai na nyuma ya hayo, msongo wa mawazo unatajwa kuwa chanzo kikuu.

Mwalimu wa Maadili katika Chuo Kikuu cha Kairuki, Abraham Mwalugeni, anasema hivi sasa changamoto ya afya ya akili kwa wanafunzi wa vyuo vikuu ni kubwa.

“Tunayo ‘challenge’ kubwa ya ‘mental health’. Wanafunzi wanajiua, wengine wanaacha shule,” anasema kauli ambayo inafungua mjadala mpana, je namna gani tutajikwamua tulipo?!.

UHALISIA UPOJE?

Kijana anapojiunga chuo ana wastani wa mwaka mmoja, miwili, mitatu hadi mitano aondoke na ‘qualification’ yake anayoitarajia.

“Masomo yana ‘demand’ kubwa pia kuna ‘presha’ yake binafsi [mwanachuo], kuna ‘presha’ kutoka kwa wazazi/walezi, pia kwa walimu ‘wana-demand’ afikie ‘pass mark’ fulani.

“Mitihani ya mara kwa mara, kwa hiyo hii inamlazimisha mwanafunzi, kufanya vitu ambavyo ni nje ya kanuni au matakwa ya kuzingatia kwa mfano kutokulala au kula vizuri,”

Kauli yake Rais wa Serikali ya Wanafunzi Chuo Kikuu cha Kairuki [KUSA Kairuki] Ayoub Daffa.

Kwa mujibu wake yote hayo huathiri afya ya wanafunzi na saikolojia yao na matokeo yake wengi pia hupata matokeo mabaya kwenye mitihani yao.

Mwal. Mwalugeni anadokeza “Labda mifumo yetu inashindwa kuwapokea [vijana] sawa sawa,”.

Kauli yake inaungwa mkono na tafiti mbalimbali nchini. Utafiti uliochapishwa katika jarida la BMC Psychiatry kuhusu wanafunzi wa vyuo Tanzania.

Unaonesha kuwa kiwango kikubwa cha wanafunzi wanaripoti dalili za ‘mental distress’.

Pamoja na utafiti huo, kuna baadhi ya tafiti nyingine zinaonesha takriban 70% ya wanafunzi wanakabiliwa na changamoto za afya ya akili kama msongo wa mawazo na wasiwasi.

Upo, utafiti uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Dodoma unaonesha zaidi ya nusu ya wanafunzi [51.8%] waliripoti dalili za mental distress.

Watafiti wanaeleza hali hiyo inaonesha ukubwa wa tatizo ndani ya taasisi za elimu ya juu.

Ndani ya Mkoa wa Mwanza, utafiti uliohusisha vyuo visivyo vya tiba ulibaini takriban 35.7% ya wanafunzi walikuwa na dalili za unyogovu .

Takwimu inayodhihirisha kwamba afya ya akili kwa vijana wa vyuo si hoja ya nadharia, bali ni uhalisia unaohitaji hatua.

MABADILIKO GHAFLA

Mwal. Mwalugeni anasema safari ya mtoto ki-elimu nchini Tanzania hubadilika ghafla anapofika chuo kikuu.

“.., kuanzia darasa la kwanza hadi la saba, mtoto huwa chini ya uangalizi wa wazazi na walezi. Akiwa sekondari, bado anafuatiliwa kwa karibu na kukumbushwa wajibu wake wa masomo.

“Lakini anapofika chuo, anajikuta chini ya utawala wake mwenyewe [utawala na maamuzi binafsi] na majukumu mapya,” anasema.

Anasisitiza “Huku chuo ni tofauti na kule msingi na sekondari, hapa hakuna anayekulazimisha kuandika, kusoma, ni wewe uwe makini na uzingatie ulichokifuata.

“Ninachokiona mimi, huyu kijana anashindwa ‘ku-transform’ maisha yake,” anaeleza Mwl. Mwalugeni.

BOOM ‘LINAWAVURUGA’

Anagusia pia suala la mikopo ya elimu ya juu [boom]. Kwa baadhi ya wanafunzi, fedha hizi badala ya kuwa msaada wa masomo hugeuka chanzo cha kuyumbisha mwelekeo.

“Akipata ‘boom’ ndiyo linamvuruga kabisa. Kuna ambao wanaacha chuo na kwenda kutumia fedha walizopata mpaka zitakapoisha ndiyo wanarudi.”

Kwa mtazamo wake, si suala la fedha pekee, bali ni ukosefu wa maandalizi ya kisaikolojia na kifedha.

Uhuru wa ghafla bila mwongozo wa kutosha huwafanya baadhi ya vijana kushindwa kusimamia maisha yao mapya.

Hapa ndipo hoja ya wataalamu na tafiti zinapokutana, vijana wengi wanaingia chuoni bila maandalizi ya kutosha.

Suala la kukabiliana na presha ya masomo, changamoto za kifedha, mabadiliko ya kijamii na upweke.

Mambo hayo huchangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa dalili za msongo wa mawazo na unyogovu.

CHANGAMOTO YA DUNIA

Kwa mtazamo wa kitaifa na kimataifa, Profesa Mstaafu wa Afya ya Akili na mshauri wa Akili Platform Tanzania, Profesa Gadi Kilonzo, anasema tatizo la afya ya akili si la vyuo na vyuo vikuu pekee.

Ni changamoto ya dunia nzima, ndiyo maana kumekuwa na juhudi mbalimbali zinazofanyika na kila nchi ili kukomboa hatma ya raia wake.

Anabainisha takwimu zinaonesha kuna watu takribani milioni 450 wanaoishi na matatizo ya akili kila mwaka, huku zaidi ya milioni moja wakijiua kila mwaka. 

Pia, takribani watu milioni 150 wanaishi na sonona [depression], milioni 25 wana tatizo la skizofrenia, milioni 28 wanaugua kifafa na takribani milioni 90 wanakabiliwa na matatizo ya ulevi wa pombe.

Kwa upande wa Tanzania, tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa matatizo ya afya ya akili yapo kati ya 0.32% hadi 31 ya wananchi.

Tafiti zinaeleza katika kliniki za magonjwa ya kawaida, mahudhurio ya awali yanaonesha 49% ya wagonjwa wana matatizo yanayotokana na msongo wa mawazo.

Mkurugenzi wa Akili Platform Tanzania, Roghat Robert, anasema vijana ndio wanaoongoza kuathiriwa na changamoto zinazoathiri afya ya akili.

"Ikiwamo hali ngumu ya uchumi, matumizi ya dawa za kulevya na kuporomoka kwa maadili," anasema.

TUNATOKAJE?

Mwl. Mwalugeni anapendekeza kuwepo kwa programu za ‘financial management mentorship’ na ushauri nasaha ndani ya vyuo vikuu.

“Kama angalau mara moja hadi nne kwa mwaka wanafunzi watapatiwa mafunzo ya usimamizi wa fedha na maisha kwa ujumla, itawasaidia na itatusaidia sana.”

Afya ya akili ya vijana vyuoni si suala la mtu binafsi pekee. Ni taswira ya mifumo yetu ya malezi, elimu na msaada wa kijamii.

Profesa Kilonzo anasisitiza kila hatua ndogo ya kuimarisha ustawi wa akili ni muhimu, ikiwemo kuanzisha huduma rafiki za saikolojia, kuelimisha wazazi na walimu.

Pamoja na kuhakikisha vijana wanapata msaada mapema kabla ya matatizo kuwa makubwa.

Daffa anasema ndiyo maana walichukua hatua zaidi kuanzisha jukwaa la KUSA YOUTH MENTAL HEALTH CONFERENCE.

“Ni jukwaa letu muhimu, linatuleta pamoja na wataalamu wa masuala ya afya na magonjwa ya akili, pia wanasaikolojia, tunajadili kwa uwazi,” anasema.

Anaongeza “Vijana tunapata kujifunza kati yetu, kuna wale ambao wamewahi kupitia changamoto basi wanatueleza, mwengine anapata cha kujifunza nia hasa ni kuijenga afya ya akili tukiwa hapa chuoni.

“Kimsingi, ‘mentorship’ ina umuhimu mkubwa, unajifunza kwa mwenzako aliyewahi kupata changamoto na unapata kitu cha kukusaidia siku za usoni.

“Moja ya tiba kubwa ni kuzungumza, mimi ni muumini kabla sijakanyaga hatua moja, mtu ambaye amewahi kukanyaga hatua ile, nitamfuata na kuzungumza.

“Alipopitia, alitokaje?, unajua hizi changamoto huja kama ‘suplize’ ila unapofanya ‘recall’ niliwahi kuzungumza na mtu kuhusu hili, alitoka namna gani, unafanya nawe unatoka salama,”.

 Kauli inayotiliwa mkazo na Mkurugenzi wa Akili Platform, Robert anasisitiza “Tunalenga kupaza sauti za vijana na kuwahamasisha kuvunja ukimya kwani ukimya hauponyi afya ya akili. 

"Ni muhimu kuwa na mifumo ya msaada, 'mentorship' na ushauri mapema,” anasema huku akibainisha suluhisho la muda mrefu ili kunusuru vijana.

Ni pamoja na kuimarisha eimu na uelewa wa afya ya akili katika jamii na vyuo vikuu, kuhamasisha utunzaji wa familia na mahusiano chanya.

Kuweka mikakati ya kutambua na kusaidia mapema vijana wanaokabiliana na msongo wa mawazo, unyogovu au hali nyingine ya kisaikolojia.

Kuongeza upatikanaji wa 'mentors', wataalamu wa saikolojia na madawati ya jinsia kwa wanafunzi wa vyuo

Hii inaashiria kuwa afya ya akili si jukumu la mtu binafsi pekee, ni jukumu la jamii nzima, vyuo, familia, wadau wa afya na Serikali.

Hatua hizo zitasaidia kuhakikisha vijana wanapata msaada, elimu na fursa za kujenga ustawi wa akili, ili waweze kufanikisha ndoto zao na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement