moja

Responsive Advertisement


Na Mwandishi Maalum

Elizabeth Marealle ambaye ni mmoja wa waasisi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), amefariki dunia. Huzuni imetanda katika mioyo ya wana-TAMWA kufuatia kifo hicho cha nguli huyo mtetezi wa masuala ya wanawake na watoto, nchini Tanzania. 

Tangazo kuhusu kifo hicho lilitolewa na Halima Shariff ambaye pia ni mwasisi wa TAMWA walioshirikiana kwa ukaribu kuanzisha Chama hicho miaka hiyo ya zamani.

'Ndugu zangu wana-TAMWA nimepata taarifa sasa hivi founder member ELIZABETH MAREALLE amefariki Arusha jana na taratibu za mazishi zinaendelea. Innalilahi wa Innaillahi Rajiun!," alisema Halima hapo jana.

Jumbe mbalimbali za majonzi zimetumwa na wana-TAMWA wakimuelezea Elizabeth alikuwa mpole, makini na jasiri na wakimtakia pumziko jema.

Mwenyekiti Mstaafu wa TAMWA Joyce Shebe amesema " Ooh mama Elizabeth. Hakika kila nafsi itaonja mauti!! Tunaumia lakini sisi ni wanadamu, tumeelekezwa kushukuru kwa kila jambo. "Tunamshukuru Mungu kwa maisha yako, hakika uliipenda TAMWA, na hata tulipokutafuta baada ya ukimya wa muda mrefu, ili uje ushiriki sherehe za miaka 36 ya TAMWA ulikubali... 

"Nilikuwa sikufahamu lakini uso wako ulinipokea kama mtu anayenijua, ulionyesha furaha yako ya kukutana na vijana wenzio wa enzi zenu!!!, hakika siku mbili zile sisi wanachama wachanga wa TAMWA tuliiona nguvu yenu na siku zote tutajivunia kazi yenu na msingi imara wa taasisi yetu mliouweka. Mungu akupe pumziko la amani mama Elizabeth! Mwendo umeumaliza," amesema.

Hapa M24 TANZANIA MEDIA tunaichapa makala yake aliyoandika enzi za uhai wake. 

Tamwa treni lililo konga mioyo ya watu kwa miaka 36

Na Elizabeth Marealle

"Jamani naipenda Tamwa imenisomesha na  imenipa fursa  mbalimbali. Na sasa mimi ni mwanachama hai nalipia ada kila mwaka." 

Haya ni maneno ya mdau ambaye si wanahabari aliyetaka watu wajue kuwa na yeye amependa kushiriki sherehe kubwa iliyoandaliwa jijini Dar es Salamu mwishoni mwa Novemba, kukumbuka miaka 36 tangu TAMWA iundwe. Na si mtu mmoja, wapo marafiki wengi wa TAMWA wanarudia maneno hayo. 

TAMWA ni nini? Ni Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania. Na kimepata sifa nchini kwa kujipambanua kuwa miongoni mwa asasi za hiari zinazopigania haki za wanawake na watoto.

Bila kuhama misingi yake ya taaluma ya  upashanaji habari; TAMWA imefanya kazi zake kwa kalamu, maikrofoni, kamera na kutumia mbinu ya uchunguzi katika harakati zake za kutetea haki za wanawake na watoto. 

Waasisi 13 walioanzisha TAMWA walitoka vyombo vyote, yaani  waandishi, watangazaji na wapiga picha za mnato na video. Lakini baadaye wigo wa uanachama  uliongezwa baada ya kukua fani ya digiti na teknolojia ya habari. Wakawepo wanawake karibu wote wanaofanya kazi katika vyombo vya habari. 

Miaka 36 iliyopita vyombo vya habari vilikuwa ni redio, magazeti na TV chache. Baada ya kukua kwa teknolojia na kuanzishwa  mitandao ya kijamii sasa hivi tunazungumzia utitiri wa vyombo vya mawasiliano. 

Kwa teknolojia ya sasa wafanyakazi wa vyombo vya mawasiliano, wapende wasipende, wanajikuta kwawa ni watoa habari walio mstari wa mbele. Na hapo ndipo unapoona kwa nini ukitaka kuuza habari ikiwa bado moto huna budi kutumia teknolojia ya mitandao ya kijamii kurusha "video clip" au ufupisho wa habari unayotaka kuiuza haraka.

Kwa hiyo usishangae kwa kuwa uanachama ni hiari kwa wana habari wanawake, TAMWA pia imejikuta ina wanachama marafiki (friends of TAMWA) kutoka kila fani. Na hilo ni jambo la afya ukizingatia usemi huu: "Wewe panda mbegu na sisi sote tule chakula." 

Hawa marafiki wameridhika. Wanaona TAMWA ni yao pia. Inafurahisha sana. Maana sherehe ya miaka 36 ilifana sana na baadhi ya vionjo ilikuwa ni  kutokana na  uwepo wa washiriki toka maeneo mengi.

Kwenye sherehe hizo za tarehe 28 hadi 29 Novemba walikuwepo wanasiasa na wana harakati na hata toka nchi jirani. Pia walikuwepo  waheshimiwa viongozi wa ngazi mbalimbali nchini  ambao nao walitamka hadharani kuwa: "na mimi ni mwana TAMWA." Tunawashukuru. Tunawakaribisha. Tunawapenda. Hivyo tuingie treni tusafiri pamoja. Asiachwe kituoni hata mtu mmoja maadamu anayetupenda. 

Treni letu la TAMWA hoyeeeee.

Picha zote kwa hisani ya TAMWA, zilipigwa katika Maadhimisho ya miaka 36 tangu kuanzishwa kwa Chama hicho.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement