Na Veronica Mrema
Umewahi kufikiri, mgonjwa anapokuwa kitandani akihitaji Tiba
Damu kwa haraka ili kuokolewa uhai wake? Ila ndani ya hospitali alipo hakuna
kundi lake la damu au kuna upungufu mkubwa wa damu?
Hali ambayo huwalazimu madaktari kuanza kuhangaika
mawasiliano kati ya hospitali moja na nyingine, au katika benki kuu ya Mpango
wa Taifa wa Damu Salama kuuliza iwapo watapata?
Ni wakati mgumu hasa pale kunapokuwa na idadi kubwa ya
wahitaji huku kiwango kilichohifadhiwa benki ya damu hakitoshelezi uhalisia.
Kwa mazingira ya namna hiyo, mara nyingine mgonjwa hushindwa
kuhimili kusubiri hadi ipatikane, kuna ambao hupoteza maisha.
“Niliwahi kukutana nalo, kuna mgonjwa alikuwa anahitaji damu aina fulani … nakumbuka ilikuwa B+ kwa wakati huo haikuwapo,”.
Kwa Adoph Jumanne
Afisa Muuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili hii si simulizi ya kusimuliwa, ni
hali anayokutana nayo kazini kwake, japokuwa si mara zote.
“Bahati nzuri Wizara ya Afya ina mawasiliano kutoka sehemu
moja hadi nyingine. Kwa mfano Muhimbili kuna
wakati tunazidiwa tunaenda lugalo.
“Tunaenda mpaka mikoani huko kuna muungano unakuta mgonjwa
anahitaji damu na wakati huo tumeishiwa,’ anasema.
Anaongeza “Inabidi tuwasiliane kujua damu itakayoendana na yeye
itapatikana wapi?
“Unakuta … mnaweza kuipata ipo mbali lakini mpaka ifike unaambiwa ameshafariki, lakini kama tungekuwa na ‘stock’ kubwa watu wanajitolea kwa hiyari ingekuwa inasaidia tungeokoa wengi zaidi,”.
JE, HALI IPOJE?
Nchini Tanzania bado kuna kundi kubwa la watu wasio na
hamasa ya kujitokeza kuchangia damu kwa hiyari.
Hali ambayo inafanya ishindwe kufikia kiwango cha asilimia
moja ya idadi ya watu wake ili kutosheleza mahitaji halisi, kama
inavyopendekezwa na Shirika la Afya Duniani [WHO].
Kwa mantiki hiyo ikiwa idadi ya Watanzania ni watu milioni
60 kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 hivyo inahitaji wastani
wa chupa 600,000 za damu salama kwa mwaka.
Lakini kwa mwaka 2025 pekee imeweza kufikia kiwango cha 71%
ya makusanyo, ni wazi bado kuna upungufu.
Makundi yanayohitaji zaidi Tiba Damu ni pamoja na wakina
mama hasa wakati wa kujifungua, wagonjwa hasa wa Siko Seli na Saratani
mbalimbali, majeruhi wa ajali hasa za barabarani na kundi la watoto.
Licha ya wakina mama kuwa miongoni mwa wahitaji wakubwa wa
damu lakini bado ni kundi linalosalia kuwa nyuma kujitokeza kwa hiyari
kuchangia damu ikinganishwa na kundi la wanaume, kulikoni?
“Baadhi wanaogopa kwa sababu ya mabadiliko ya ki-mwili,
uwoga tu… kwa sababu si unajua sisi kila mwezi tunapata hedhi, hivyo mtu
anaogopa anahisi atapungukiwa zaidi,” anaeleza Anitha Magese.
Suala hili halina ukweli wala ushahidi wowote ule wa
kisayansi, ni mtizamo tu ambao umejengeka miongoni mwa wanawake.
Kuna wengine ambao pia wana mitazamo kwamba mwanamke anapojitolea damu hujiweka kwenye hatari ya kupata magonjwa mbalimbali, hii huwarudisha nyuma juu ya suala la kuchangia damu.
‘NGUVU YA ZIADA’
“Watu wengi bado wana imani zao tofauti tofauti nadhani tuna
kazi kubwa kama watu wa afya kuendelea kuelimisha jamii,”
Kauli yake Daktari Rhobi Jeremiah, anaongeza “.., ukweli ni kwamba jamii yote inatakiwa ijue na ichukue hatua. Suala la uchangiaji damu, kina mama tuna hurum.
“Tuna upendo na mara nyingi tunatamani kuleta mabadiliko
ambayo yatagusa jamii moja kwa moja.
“Wengi wanaogopa kwa sababu ya uwoga, [ile] sindano kwamba
watazimia, [lakini] wakina baba wanaona tunaweza [‘why not’].
“.., kina dada, kina mama tunaweza kufanya kitu. Ule uwoga ututoke kama wanawake.
“Sisi wataalamu wa afya tuna kazi kubwa kuendelea
kuelimisha. Wakina mama wasiogope pale wanapoelimishwa wachukue hatua.
Ni miaka minne mfululizo sasa Anitha amekuwa akijitolea damu
na anashuhudia wazi kwamba hajawahi kupata upungufu wala ugonjwa wa aina yoyote
ile.
“Nilianza mwaka 2022 baada ya kuhitimu kidato cha nne … mama
yangu tu alikuwa anaenda kuchangia akaniambia Anitha twende tukachangie damu,
nikamwambia naogopa.
“.., akaniambia usiogope ni kawaida tu. Hiyo ndiyo ilikuwa
siku yangu ya kwanza kuchangia damu, ilikuwa kambi za kidini.
Anaongeza “Hiyo siku nikachangia nilikuwa naogopa sema sikujisikia
utofauti wowote ule, nilijisikia kawaida.
“Tangu hapo kwa ‘influence’ ya mama yangu,ni mpenzi sana wa
kuchangia damu, alikuwa anasema tuchangie damu kwa kuwa watu wengi wana uhitaji
wa damu, hivyo nikapata ule moyo wa kujitoa.
“Sikuona utofauti wowote kwenye kutoa damu, niliona kawaida tu. Hamna kitu chochote kilichonitokea. Tangu hapo nikawa mchangiaji wa damu mpaka sasa ni mara yangu ya tano,” anasimulia.
VIJANA NA MTINDO WA
MAISHA
Kikwazo kingine kinatajwa kwa kundi la vijana kwamba wengi
wao huogopa kujitokeza na kujitolea damu kwa hiyari wakihofia hali zao kiafya.
Johnson Focus ni miongoni mwa wachangia damu wa hiyari anafichua
kwa kina “Moja ya changamoto kubwa ambayo tunakutana nayo vijana wa kiume kwa
upande wetu ni uwoga, hofu na presha.
“Vijana wengi wa kiume kutokana na kujihusisha na mahusiano
bila kupata elimu, kuwa na wapenzi wengi inawapelekea kuwa na hofu.
“Hajui sasa mpenzi wangu yupi anaweza akawa na changamoto
fulani, fulani. Kwa hiyo kwenye ‘ishu’ ya kwenda kuchangia damu anajua nitapimwa
UKIMWI na magonjwa mengine.
Anaongeza “Kwa hiyo kutokana na kujua kwamba nitapimwa
ukimwi, anakuwa na mawazo ikitokea nina ukimwi? Anakuwa na presha.
Hoja hii inaungwa mkono na Mkurugenzi wa Bone and Blood
Foundation Neema Mohamed anasema “Vijana wapo wanachipukia katika mahusiano …
mwingine … anakuuliza mnapima UKIMWI?.
“Unakuta ujana unamuita, hofu inamuandama, mambo ya kupima
anashindwa kujiamini, tofauti na watu wazima unakuyta ameoa, ana watoto
anajisimamia na inakuwa rahisi kuchangia damu mara kwa mara”.
Mnandwa Mnandwa anaongeza “Elimu imekosekana jinsi ya
kuchangia damu, tumekuwa na akili potofu.
“.., [kwenye jamii] kwamba unapochangia damu leo unapofikia
kipindi fulani umeshindwa kuchangia kwa wakati
unaweza kupata madhara fulani.
“Sasa zile ‘story’ [potofu] nahisi zikiondoshwa na elimu ikapatikana sahihi, nahisi tutapata wimbi kubwa sana la vijana watahamasika na kuchangia damu na tukaokoa maisha ya watu wengi,” anasisitiza.
Ni mara ya nane sasa anachangia damu kwa hiyari yake
mwenyewe, anasema “Sikuhamasika kwa sababu nilishawahi kupata tatizo au ndugu
yangu alipata tatizo hapana.
“Tangu elimu ya sekondari muda ambao umri, kimo na kilo
ziliruhusu nilianza uchangiaji damu. Kilichonisukuma ni moyo.
“Kwa sababu tunawachangia wenye uhitaji, sikuweza tu kuanza
niliambiwa elimu kuna watu wana shida sana na wanahitaji kupata faraja kutoka
kwetu.
“Ule moyo wa upendo kwamba ninachotoa kinaenda kuokoa watu,
nilipata hamasa,” anasema.
Neema anasema suala la elimu kwa vijana ni la kutilia mkazo
kwani ikiwa watafikiwa zaidi ni wazi kwamba itakuwa rahisi kwa Tanzania kufikia
100% ya mahitaji yake ya damu.
“Kwa Bone and Blood Foundation watu wetu wa hiyari kundi ni
miaka ya vijana kuanzia 25 hadi 45 ni sawa na kusema 90% ndilo lililobeba ile
data base yetu.
“Imefikia sasa kupitia elimu unaweza kuamka asubuhi ukakuta
mtu amekutumia ujumbe leo naenda kuchangia damu,” anasema.
Hata hivyo changamoto inasalia si asilimia kubwa ambao
wanaendelea kuwa na uendelevu wa kuchangia kwa hiyari.
“Vijana ni watu ambao bado wanajaribu tofauti na lile
lingine la watu wazima, leo ukimpa elimu atakuja na kuchangia ila kesho na
michakato ya maisha inakuwa inaingia na kutoka kwa hili kundi.
“Sababu nyingine watu wanahama… tunakosa ‘follow-up’ na kule anakoenda anaosa hamasa ni lazima utamkosa,” anasema.
Johnson anashauri madaktari na wataalamu wa afya pia kutumia
njia rafiki zaidi ya jinsi ya kuwasiliana na kundi la vijana ili waendelee
kupata hamasa ya kujitokeza na kuchangia damu kwa hiyari.
“Changamoto pia kwa madaktari wajue kizazi chetu si kama
kile cha mwaka 1900 vile ambavyo walikuwa wanaweza kuongea nao,”.
Anaongeza “Sisi kizazi chetu kina mabadiliko, kuna lugha ya
kwetu [Genz], kuna u-tofauti hata wa misimu na maneno mbalimbali.
“Kuna lugha ambayo ukiongea na kijana mtaelewana. Lakini
ukiongea na mtu mzima hamtaelewana,”.
Msisitizo zaidi unawekwa pia, kuongeza nguvu ya hamsa na mawasiliano kwa njia mbalimbali za
kidigitali ili kuvutia kundi hili la vijana wa kizazi kipya, kujenga desturi ya
kuchangia damu kwa hiyari.

Chapisha Maoni