Na Veronica Mrema – Afrika Kusini
Uhai
wa dunia hadi sasa ni takriban miaka zaidi ya bilioni 3.6 kwa mujibu wa tafiti
mbalimbali zilizofanywa na wanasayansi, hii ni sayari yenye historia isiyo na
kifani.
Kuna
shahidi za kusisimua, tafiti zinaeleza kuna miamba ya zamani zaidi duniani,
ambayo ipo mbali upande wa Mashariki mwa Australia na mengine ipo Kaskazini mwa
Perth.
Miamba
mingine ipo Kusini mwa Afrika karibu na Kruger Park katika eneo la Barberton.
Wanasayansi
wanaeleza huko kwenye maeneo hayo kuna ushahidi wa awali wa maisha ya kale,
ikiwa ni pamoja na mimea vile vile wanyama hadi zana zilizowahi kutumiwa na
binadamu wa kale.
Kwa
mantiki ya shahidi hizo za tafiti za wanasayansi, historia inaonesha wigo wa
maisha kwa miaka zaidi ya bilioni 3.6 kufikia sasa.
Chuo
Kikuu cha WITS kilichopo hapa Pretoria, Afrika Kusini, jitihada kubwa zilifanyika
katika tafiti na bado zinaendelea kufanyika, wakiangazia kwa kina asili ya
binadamu, duniani.
M24 TANZANIA MEDIA imefika ndani ya chuo
hiki, miongoni mwa vyuo vikongwe zaidi Barani Afrika.
Mafuvu
ya viumbe vya kale, mifupa, nyaraka nyingi zenye vielelezo zipo hapa, mengi
tumejionea na tumeelezwa, ndiyo msingi wa kuandikwa kwa makala haya.
Desemba
5, 2025 tupo ndani ya chumba maalum cha makumbusho ya kale, ambamo pia ni
sehemu ya maabara maalum ya chuo Kikuu cha WITS.
Hii
ni ziara maalum ya ki-mafunzo, ikiwa ni sehemu ya shughuli zilizoandaliwa na waandaaji
wa mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani [WCSJ -
2025].
Kwa
mara ya kwanza WCSJ umekutanisha waandishi wa habari wa masuala ya sayansi
kutoka nchi zipatazo 80 duniani.
Chuo
hiki kimeweka jitihada kubwa, ikiwamo taasisi maalum Evolutionary Studies
Institute [hapa tulipotembelea].
Hii
ni moja ya sehemu bora zaidi duniani zinazochunguza historia ya maisha ya
binadamu na dunia kwa ujumla.
Taasisi
hii ina wanyama na mimea ya ajabu kutoka kipindi cha kale, lakini moja ya
maeneo yake muhimu ni ‘evolusheni ya hominid’.
Simulizi
ya makala haya imebeba maelezo ya msingi kabisa, ya kuvutia ambayo tulipatiwa
na Prof. Bernard Zipfel ambaye alikuwa mwenyeji wetu katika ziara hii, karibu ufutane nasi.
UNDANI WA HOMINID
Unaweza
sasa kuwa unajiuliza ni kitu gani hiki, ndugu msomaji wetu, Hominid ni kiumbe
aliyekuwa anakalia miguu miwili na aliishi kwenye miti.
Kiumbe
huyu alikuwa na maumbile yanayofanana kwa ukaribu sana na nyani pamoja na binadamu
kama ilivyo sasa.
Prof.
ambaye alikuwa mwenyeji wetu katika ziara hii anasema kiumbe huyu aliishi takriban
miaka milioni 15 iliyopita.
Kwa hiyo tumetokana na kiumbe huyu mmoja kutoka hapo ‘mizizi’
[vizazi] mbalimbali ya binadamu na nyani ilitokea.
Nyani
wa kisasa na binadamu wa kisasa wote ni sehemu ya mchakato huu wa ‘evolusheni’.
Kuna tafiti zinaeleza Hominid wa zamani zaidi aliyeonekana hadi sasa ni wa
takriban miaka milioni 7.
Sampuli
yake imepatikana Chad, Afrika
Magharibi na maumbile ya awali [mifupa] yamepatikana Uruguay, Kenya, Ethiopia,
na kusini mwa Afrika.
Hominid
wa zamani zaidi utakaoonekana katika maktaba ya hapa WITS ina takriban miaka milioni 3.5.
Jambo linaloonekana kama miaka kidogo pale ikilinganishwa na
muda maisha yamekuwa duniani, milioni 3.5 dhidi ya bilioni 3.6, kwa mujibu wa Prof.
BINADAMU WA SASA
Kwa
historia ya mwanadamu, kuna sehemu ya ‘Origin Center’ ndani ya Chuo Kikuu
cha WITS ambamo inasimulia hadithi ya binadamu wa kisasa [tutaeleza katika makala ijayo].
Binadamu
wa sasa wamekuwa duniani kwa takriban miaka
300,000 tu. Hominid na binadamu wa sasa wote asili yao ni Afrika, baadae wakahama kwenda Asia,
kisha Ulaya.
Prof.
anasema kwa kuwa Australia na Marekani zilikuwa mbali sana, binadamu wa sasa
walifika pale miaka 40,000 iliyopita.
Ni
binadamu wa sasa tu waliokuwa na uwepo wa mbali, hominid hawakuwahi kuenea nje
ya Asia na Ulaya, isipokuwa Neanderthals na baadhi ya spishi zinazofanana.
SIRI YA MAUAJI YA KALE
Upo
ushahidi wa moja ya mifano ya kuvutia ambayo ni ‘Taung Child’, huyu ni kiumbe mdogo umri wake ni takriban miaka
milioni 2.5, ki-historia jina lake ni Australopithecus africanus
Fuvu
lake lipo hapa ndani ya Chuo Kikuu cha WITS huyu alikuwa mtoto wa takriban
miaka mitano, na alikuwa hominid pekee aliyeonekana pale ‘Taung’.
Uchunguzi
wa kisayansi umeonesha kwamba Taung Child aliuwawa na tai, jambo ambalo
lilikuwa siri kwa muda mrefu.
Watafiti
Profesa Lieberger na Profesa Ron Clark waliangalia alama za mapigo nyuma ya
macho na alama ndogo za kuungua kwenye mfupa.
Uthibitisho
ulipatikana baada ya Profesa Berger kuona nyani waliouawa na tai waliokuwa na
taji, ambapo makucha ya tai yalipita kwenye sehemu ya nyuma ya macho.
SIRI
ILIJULIKANA VIPI?
Tai hao walichukua ubongo wa hominid huyo kwa sababu ya
protini nyingi. CT scan na uchunguzi wa makini wa mfupa unaonesha alama za
makucha na kuchomwa katika sehemu yake ya uso.
Sababu
za ki-sayansi za kuchunguza mtoto mdogo ni nyingi: ukubwa, mdogo wa ubongo,
kuwa ni mtoto, na sababu za kisiasa.
Wakati
huo, mtazamo wa kikoloni wa kifalme ulikuwa binadamu lazima atoke Ulaya.
Wanasayansi wa wakati huo walikataa kwa muda mrefu asili yetu Afrika.
Ilibidi
kusubiri takriban miaka 25 kabla ya kushughulikia ushahidi huu vyema.
Leo, bila shaka, tunajua binadamu anatokea Afrika.
AFRIKA MASHARIKI
Kuna
ushahidi mwingine wa kuvutia wa hominid wa awali [maisha ya binadamu wa kale],
sampuli ya kwanza ya Australopithecus afarensis kutoka
Afrika Mashariki.
Pia
kuna Paranthropus robustus kutoka Afrika Kusini na ushahidi wa
viumbe Australopithecus africanus waliopatikana kusini mwa Afrika.
Ushahidi
huu unaonesha kwa wazi kuwa Afrika ni asili ya mwanadamu wa awali.
Aidha,
kwa binadamu wa sasa ushahidi wa molekuli unaonesha protini na vinasaba vya
mwanadamu vinathibitisha kuwa binadamu wote wanatoka Afrika.
Ingawa
‘fosili’ [mabaki ya mifupa ya viumbe vya kale] nyingi zinapatikana mashariki na
kusini mwa Afrika, si lazima kwamba pale ndiko walikokuwa binadamu wote.
Bali
pale ndipo ‘fosili’ zilipohifadhiwa. Hivyo, wanapaita maeneo haya ‘Cradle of
Humankind’, hii maana yake ni pale
ambapo historia ya mwanadamu ilihifadhiwa vyema.
‘LITTLEFOOT NA HOMO NALEDI’
Ndani
ya maabara hii kuna hominid mwingine wa ajabu aliyeitwa Australopithecus
prometheus, au Littlefoot, aliishi duniani takriban
miaka milioni 3.6 iliyopita.
Mfupa
wake wa mguu ulipatikana kwanza na Profesa Ron Clark, na mfupa mzima
ukapatikana baada ya miaka 21 kutoka pango la Stankfontein, nje kidogo ya
Johannesburg.
Littlefoot ni mfupa kamili zaidi
wa Australopithecus duniani na bado
unasomwa na wanasayansi.
Upo
mfano mwingine uliochapwa mnamo 2008, kutoka Malaka, pamoja na Australopithecus
prometheus, ulio na umri wa takriban miaka 2.6 hadi 1.5.
Mfano
huu bado unasomwa kwa makini na wanasayansi, pamoja na sampuli nyingi mpya nazo
zinaendelea kuongeza uelewa wao kuhusu hominid hao.
Mfano
huu ni mtoto wa kiume wa takriban miaka 11 na upande mwingine kuna mwanamke
mzima.
Ndani
ya makumbusho ya WITS pia wana Homo naledi, sampuli zilizopatikana mnamo
mwaka 2013, zikiwa na zaidi ya sampuli 3,000, katika pango dogo takriban
mita 30 chini ya ardhi.
Wanasayansi
wanasema Homo naledi ni [viumbe] wa kuvutia kwa sababu walikuwepo takriban miaka
240,000 iliyopita, wakati binadamu wa sasa tayari walikuwa duniani.
AFRIKA MSINGI WA HISTORIA
Historia
ya mwanadamu ni ya kipekee yenye maajabu mengi, yanayoenda sambamba na msururu
wa shahidi za kisayansi usio na kifani.
Umeona
msisimko wake tangu hominid wa milioni
7 hadi binadamu wa sasa wenye miaka
300,000 ndani ya sayari ya dunia.
Historia
hii inaonesha ukuaji wa akili, sura, mwili na mabadiliko yake ya maisha. Afrika
si tu asili ya mwanadamu alipoanza, bali
ni msingi wa historia ya binadamu wa sasa.
Unapoanzia
pale Barberton, Taung, Stankfontein, Malaka hadi Homo naledi, unaona jinsi historia
ya dunia inatufundisha kwa ajabu na kutupa nafasi ya kuelewa sisi ni wakina nani!.
Historia
hii ni changamoto, ya kuvutia na yenye mvuto mkubwa kwa kila mtu anayetaka
kuelewa asili yetu na safari ya binadamu.
Mfululizo
wa simulizi kuanzia jicho la mwanadamu mdogo lililokatwa na tai, hadi Littlefoot na Homo naledi.
Ushahidi wa tafiti za ki-sayansi na ki-historia unaendelea kutufundisha kuwa historia ya mwanadamu ni tajiri, yenye ushahidi wa kisayansi na ajabu zisizoisha.



Chapisha Maoni