Unapoona leo hii mabadiliko ya hali ya hewa yasiyo ya
kawaida, ujue basi kuna kundi kubwa la watu wanaoumia ki-afya, ki-jamii na hata
ki-uchumi.
Ni hivi miaka ya zamani wazee wetu waliweza kung’amua kwa
urahisi kwamba huu ni msimu wa jua la kawaida au la utosi.
Je? ni msimu wa joto la kawaida, la kati au kali, vivyo
hivyo kwa upande wa mvua ni msimu wa vuli, masika na wakaweza kuishi vema kulingana na hali husika.
Kwa miaka ya karibuni, licha ya ukweli kwamba kuna maendeleo makubwa ya teknolojia na vifaa vya kisasa zaidi vya kufuatilia hali ya hewa.
Lakini binadamu tunashuhudia mabadiliko ya
tabianchi yanayoleta athari kubwa katika mifumo ya hali ya hewa na ikolojia ya
dunia.
“Ni hali ngumu, kwetu ukiamua kulima zako mahindi kwa
mfano, mara mvua haiendelei inavyopaswa, hivyo unakosa mavuno,” anasema Karim Mwaituza
Mkazi wa Kimanzichana, nje kidogo ya Mji wa Dar es Salaam.
Ripoti ya mwaka 2024 ya Mamlaka ya Hali ya Hewa [TMA]
inaeleza Tanzania ilikumbwa na hali ya
hewa isiyo ya kawaida.
Ikiwa ni pamoja na ongezeko la joto kali na mvua nyingi
hali ambayo inaashiria athari za mabadiliko ya tabianchi.
Ni hali ya hatari, Ripoti ya mwaka 2024 ya Shirika la Hali
ya Hewa Duniani [WMO] inaeleza kipindi cha miaka kumi mfululizo [2015 - 2024]
kuna rekodi ya kasi ya ongezeko la joto duniani.
WMO inatoa tahadhari kali zaidi kuhusu kasi hiyo, msisitizo ukiwekwa hali hiyo inachochea athari
kubwa kwa maisha ya watu, mazingira na uchumi kwa ujumla.
Kiwango cha bahari nacho kimeendelea kuongezeka kwa kasi pia na mabadiliko
hayo yanatarajiwa kuwa ya kudumu kwa mamia ya miaka ijayo.
Joto la bahari linapozidi kuongezeka si jambo jema kwani hali hiyo inazidi kuathiri mifumo
ya hali ya hewa na maisha ya baharini.
‘MIILI
YETU INALIA’
Makala haya yatajikita zaidi kuangazia athari za mabadiliko
ya tabianchi kwa kundi la watu wanaoishi na ugonjwa wa Siko Seli.
“Miezi kadhaa Dar es Salaam tulishuhudia mvua ambazo si
kipindi chake pia joto kali sana, mimi ninayeishi na ugonjwa wa Siko Seli
inanigharimu,”.
Kauli yake Neema Mohamed ni miongoni mwa vijana nchini Tanzania wanaoishi
na ugonjwa huo adimu ulio katika kundi la magonjwa ya damu na magonjwa yasiyoambukiza [NCDs].
Kila mwaka Tanzania watoto wapatao 8,000 hadi 11,000
wanazaliwa na ugonjwa huo, kulingana na tafiti zilizowahi kufanywa na Chuo
Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili [MUHAS].
Kabla ya athari za mabadiliko ya tabianchi ilikuwa rahisi
kwa wenye ugonjwa wa Siko Seli kujua hali fulani itatokea katika kipindi gani.
Anaongeza “Tulikuwa tunajua joto litakuja kwa kipindi
fulani baada ya hapo mvua. Baada ya hapo kipindi fulani tena.
“Sisi tunavyoishi tunakuwa na 'balancing' [ili kuepuka
maumivu makali ya viungo vya mwili / crisis].
“Lakini sasa ni tofauti. Kipindi cha nyuma tumeshuhudia
joto kali sana ambalo limepeleka kupoteza maji mwilini,” anasema
Neema.
NINI
HUTOKEA?
Madaktari Bingwa wa Magonjwa ya Damu wanaeleza si kila mgonjwa
wa Siko Seli muda wote hupata maumivu, lakini ni pale tu kunapokuwa na vitu
vinavyopelekea maumivu makali kutokea.
Kwa lugha ya kitaalamu wanaita vitu hivyo ‘triggers’ na
mojawapo ya vitu hivyo ni mabadiliko ya tabianchi.
Kwa mfano kunapokuwa na joto kali sana au baridi sana au pale mgonjwa wa Siko Seli anapokuwa sehemu yenye oksijeni ndogo anaweza kupata maumivu makali yasiyoelezeka.
Kitaalamu wanaita hali hiyo ‘crisis’ na inaweza kuwa ya muda mrefu na yakamsumbua mno mgonjwa husika na kulazimika kuuguzwa mara kwa mara.
Kuna athari za moja kwa moja yanapotokea mabadiliko ya
tabianchi na ongezeko la vipindi vya ‘crisis’ kwa mgonjwa wa Siko Seli.
M24
TANZANIA Media imefanya mahojiano ya kina na Dkt. Emmanuel Kataga
kutoka Program ya Siko Seli Program ndani
ya MUHAS.
Awali anachambua namna ilivyo utofauti kati ya seli
nyekundu za damu kwa mtu asiye na Siko Seli na yule mwenye ugonjwa wa Siko
Seli.
Uhalisia seli nyekundu za damu za mtu asiye na ugonjwa zina
umbo la duara kamili, ambazo huweza kuishi hadi wastani wa siku 90 ndipo hufa
na kuzaliwa nyingine.
Lakini seli nyekundu za damu kwa mgonjwa wa Siko Seli ipo
katika umbo la nusu duara mfano wa ndizi / mundu / nusu mwezi na hufa kwa wastani wa ndani ya siku 10.
MFUMO
MZIMA
Anasema ule ukamilifu wa seli nyekundu ya damu katika umbo
la duara huzifanya kuwa na uwezo wa kupitika kwa urahisi katika mishipa ya damu
hata kama ni midogo.
“Ile mishipa ya damu ni midogo kuliko size ya seli nyekundu
za damu na seli hizo zina uwezo wa kujikinga na kupita bila shida.
“Lakini sasa kwa zile za mgonjwa wa Siko Seli kwa kuwa zina
shida, zinakuwa na umbo nusu duara zinapoteza ule uwezo wa kufanya zipite
kirahisi kwenye mishipa ya damu,” anasema.
Seli hizo hushindwa kujikunja ili kupita kwenye mishipa ya
damu na kukwama njiani, hali hiyo inapotokea sehemu husika hukosa damu na
oksijeni pia.
“[Hali hiyo] ndiyo huleta maumivu. Pia hizi seli ambazo
zipo kama ndizi zinakuwa zina ule uwezo wa kushikana [kunatana] zenyewe kwa
zenyewe.
“[Lakini seli] za kawaida haziwezi kushikana, kwa hiyo zinaposhikana seli za siko seli zinatengeneza mrundikano wa seli nyekundu za damu zilizokwama kwenye mshipa wa damu,”.
VIPINDI
VYA HOFU
Kwa kuwa pia seli hizo hufa mapema ndani ya muda mfupi ndiyo maana wagonjwa wa Siko Seli wengi hupungukiwa damu mara kwa mara na kuhitaji huduma ya kuongezwa.
Jarome [si jina lake halisi] ameieleza M24 TANZANIA Media kwamba sasa amekuwa na vipindi vingi vya maumivu
ya mwili tofauti na miaka mitatu nyuma.
“Ni hali inanipa hofu juu ya mustakabali wa maendeleo yangu
kimasomo, kwa sababu nalazwa mara kwa mara,” anasema.
Anaongeza “Wananichoma sindano kupunguza maumivu, nashindwa
kwenda shule, nimeelekezwa kuzingatia unywaji maji ya kutosha, mlo kamili na
dawa za hydroxyulea, huwa naongezwa damu pia”.
Neema anasema kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa kuna kipindi baadhi yao hushindwa kabisa kwenda shughuli zake za kila siku kujitafutia kipato au za kujumuika na makundi mengine ndani ya jamii.
"Kwa sababu ya jua kali kupita kiasi [unakuta] maeneo ninayokwenda ukisema utoke nje, jua utakalokutana nalo ukirudi kichwa kinauma, viungo vinauma na ukijiangalia unajiona kabisa huna maji.
“Tunapata maumivu ambayo kungekuwa hakuna mabadiliko ya
tabianchi vingezuilika,” anasema.
Mwingine anaongeza hoja “Kutokana hiyo changamoto
tumejikuta kuna ile hali kama kudhoofu ambayo imepelekea nashindwa ku-balance
[niishi namna gani hasa],”.
“Kwa sababu sijui hili joto litakwenda kwa muda gani, hii
hali ya mvua itakwenda kwa muda gani?.
“Kwa hiyo imetupelekea kupata msongo wa mawazo [yaani kuna
kule kujiwazia na kufikiri zaidi kuhusu hali ya miili yetu.
Neema anasisitiza “Sasa hivi ukilala usiku [kuna hali ya joto
kali] lakini usiku wa manane inakuja baridi [au] inakuja mvua.
“Unajikuta ulivyoingia kulala ulijua mavazi hayo
yatakusaidia mpaka unaamka,”. Pale mabadiliko hayo yanapotokea huhisi baridi
kali, mwili hupata vichomi, huhisi maumivu makali.
MALARIA
& ‘INFECTIONS’
Changamoto nyingine ambayo hivi sasa imekuwa ikiwakabili
mara kwa mara watu wenye ugonjwa wa Siko Seli ni kupata maambukizi mbalimbali
ya magonjwa.
Tathmini ya hivi karibuni inaonesha wengi wamekuwa wakiripoti
katika vituo mbalimbali vya afya kufuata matibabu.
Dkt. Emmanuel anasema “Upande wa Dar es Salaam [tunaona] wagonjwa
wengi wanakuja kwa sababu ya kupata mara kwa mara vipindi vya maumivu na
kupungukiwa damu sana.
“Kipindi cha joto wanakuwa wagonjwa wengi wale ambao
hawazingatii matumizi ya maji mara kwa mara.
“Mabadiliko ya tabianchi yanakuja na kuongezeka kwa
magonjwa mbalimbali,” anasema.
Anataja mfano malaria, kwamba wale vimelea vya wadudu [mbu]
huzaliana kwa wingi hasa sehemu yenye joto.
“Hivyo, kipindi cha joto [wagonjwa wa Siko Seli] wanapata malaria
sana na tunafahamu malaria huathiri seli nyekundu za damu.
“Sasa kumbuka huyu ni mgonjwa seli zake nyekundu zinakufa
mapema na akipata malaria athari inakuwa kubwa zaidi,” anabainisha.
Anasisitiza “Anapata kupungukiwa damu sana na kuhitaji
kuongezwa mara kwa mara.
Anasema kwa kipindi cha miezi mitatu [kabla ya makala haya
kuchapwa] kliniki ya Mwananyamala na Amana wamepokea idadi kubwa ya wagonjwa.
“Wengi wanakuja na ‘infections sign’, malaria, damu ipo
chini walihitaji kuongezwa damu wengine kulazwa.
“Wengi pia wamekuja kabla ya muda wao [wa kurudi hospitali
kwa tarehe waliyopewa] kwa sababu ya maudhi wanayopata,” anabainisha na kuongeza,
“Kwa mwezi katika kliniki ya mwananyamala kuna wagonjwa
zaidi ya 100 wanaofika kliniki ya kawaida.
“Ukiangalia kuna kama 15 walikuja na maudhi / malalamiko ya
kupata ‘crisis’, kuna walioletwa wakiwa ‘serious’.
MAHITAJI
YA TIBADAMU
Wagonjwa wa Siko Seli ni kati ya wahitaji wakubwa wa
tibadamu, kwani mara kwa mara hupungukiwa na hivyo kulazimu kuongezewa tena
hospitalini.
Neema ndiye Mkurugenzi Mtendaji wa Bone and Blood Foundation,
taasisi isiyo ya kiserikali ambayo inajihusisha na uelimishaji jamii kuhusu
ugonjwa huo pamoja na kuhimiza uchangiaji damu.
Ndani ya taasisi yake anashuhudia ongezeko kubwa la
mahitaji ya damu kwa kundi la wagonjwa wa Siko Seli na wakati mwingine hata
wahitaji watokanao na magonjwa mengine.
“[Mahitaji] ni makubwa, 2021 tulipoanza ulikuwa unajua
ikifika kipindi cha Jan-March huwa kuna changamoto ya damu.
“Kwa sababu Desemba watu wengi hawachangii kwa sababu
wanakuwa wapo mapumziko ya likizo, pamoja na kundi la wanafunzi ambao ni
wachangiaji shule na vyuo huwa vimefungwa.
“[Hivyo] kunakuwa na uhaba wa damu, ni hali inayotambulika,”
anasema lakini sasa ni tofauti kwani kuna changamoto kubwa katika benki yao ya
damu, uhitaji umeongezeka mara tatu zaidi.
Anahesabu hiyo ni miongoni mwa hasara/athari za mabadiliko
ya tabianchi kwani kundi la watu wanaochangia halipo na kundi la wanaohitaji
damu ni kubwa.
“[Kwa mabadiliko ya hali ya hewa] wachangjia pia wanapata
changamoto, unakuta kuna ambao hawana afya nzuri kuweza kuchangia, unakuta
miili yao imepungukiwa maji.
“Kuna ongezeko la wahitaji wa damu, napokea simu nyingi mno, miezi mitatu sasa, changamoto ni kubwa si tu kwa wagonjwa wa Siko Seli, pia kwa wenye magonjwa mengine,” anasema.
Suala la mabadiliko ya tabianchi na athari zake kwa wagonjwa wa Siko Seli ni suala linalomgusa Mkami Wanyancha Mkazi wa Tabata, Msomi wa kozi ya Famasi katika Chuo cha Noble.
Anaishi na rafiki yake anayekabiliwa na ugonjwa huo anasema "Kuna changamoto anapitia, jua likiwa kali joto linapozidi anapoteza maji, anazidi kupata matatizo, maumivu makali.
"Huwa namshauri anywe maji ya kutosha na kuepuka safari zisizo za lazima, kwenye baridi napo huwa na changamoto namuhimiza kuvaa nguo nzito, ili asipate madhara kama kupooza mwili," anasema.
Dkt. Emmanuel anasisitiza “Kuna kipindi joto lilikuwa kali, [wagonjwa] walilalamika kupata maumivu makali, tunawapa dawa ya ‘hydroxyulea’ inasaidia kupandisha kiwango cha damu kwa mgonjwa wa Siko Seli.
“Inasaidia kuliko yule ambaye hatumii, tunawahimiza pia
kuzingatia unywaji maji ya kutosha hata ikiwa hawahisi kiu, kwani yanawasaidia
mno,”.
Anashauri pia wale ambao bado hawajaingia kwenye mahusiano
ya ki-mapenzi na ndoa wapime vinasaba vyao kujua hali zao mapema.
“Tunajua huu ni ugonjwa wa kurithi na ukiangalia Tanzania
ni nchi ya tano dunia kati ya zenye wagonwja wengi wa Siko Seli,
“Hatupo kwenye ‘position’ nzuri [hivyo] tuangalie namna ya
kukinga tusiendelee kupata wagonjwa wengi wa Siko Seli.
“Tuweke huu utaratibu watu kupima mapema kabla hawajaamua kupata mtoto / watoto, kliniki ya wakina mama na wajawazito [ni vema, napo] wapime vinasaba,” anashauri.
Mkami anashauri pia jamii kuzingatia utunzaji wa mazingira ili kuepuka athari zaidi za mabadiliko ya tabianchi.
"Uharibifu wa mazingira unaweza kusababisha kuharibika kwa mazingira, o-zone layer inaharibika na kusababisha joto kuwa kali, na kuchangia athari nyingi za ki-afya ikiwamo kundi la wagonjwa wa Siko Seli.
Chapisha Maoni