Na Veronica Mrema
Ni mtoto mwenye umri wa miaka 15 sasa, Sabrina alizaliwa
na tatizo la mtindio wa ubongo, tatizo la macho pia anaishi na ugonjwa wa Siko
Seli.
“Nilijifungua kabla ya wakati, alichelewa kulia na
kutokulia kwake kulisababisha kupata ulemavu wa mtindio wa ubongo,”.
Simulizi hiyo inatolewa na Rehema Kitindi ambaye ni mama
mzazi wa Sabrina, tulipomtembelea hivi karibuni nyumbani kwao, Mbezi Makabe
nje kidogo ya Mji wa Dar es Salaam.
“Tuliruhusiwa kurudi nyumbani aliendelea vizuri ila
alipofikisha umri wa miezi miwili alipata homa kali ya degedege, alilazwa
Hospitali ya Taifa Muhimbili [MNH],” anasema.
Anaongeza “Alipungukiwa damu, kwa mara ya pili walimpima
tena na kuona ana ugonjwa wa Siko Seli.
“Baada ya miezi sita walimpima tena ili kujiridhisha na
awamu hii tena walithibitisha amezaliwa na ugonjwa wa Siko Seli.
Anasema akiwa na umri wa miezi sita ndipo aligundulika ana
matatizo ya macho, alikuwa haoni, ilibidi afanyiwe upasuaji na kupatiwa miwani
ya tiba.
UPENDO
WA MAMA
Rehema anasimulia “Akiwa na mwaka na miezi minane, mwanawe
alipata ‘strock’ ikawa changamoto nyingine katika kumuhudumia.
“Lazima nimbebe na ninachoka kwa sababu ameongezeka uzito
sasa. Ilifika wakati hata mazoezi ile ‘speed’ ikarudi nyuma, maendeleo yake
yakarudi nyuma.
Pamoja na yote hayo mwanamama huyu shupavu anamshukuru
Mungu kumpatia mtoto Sabrina kwani anampa ujasiri mpya kila siku kupambania
maisha ya familia yake.
“Namshukuru Mungu ameendelea vizuri akiwa na ‘strock’, Siko
Seli, na mtindio wa ubongo alionao.
“Ana uhitaji wa vitu vingi, kliniki niliendelea ila kwa
kuwa anakua nikawa na maumivu ya mgongo, tuna changamoto ya usafiri.
“Sina shughuli yenye kuniingizia kipato kuweza kumuhudumia
huyu mtoto kwa kila kitu, kutoka nyumbani hadi kituoni ni mbali, inabidi
nimbebe mgongo.
Anaongeza “… wakati mwingine sina hela ya usfafiri wa
bodaboda hiyo hali ilifika hatua naumia.
SIKUMFICHA
NDANI
“Nikaendelea na kliniki ya Siko Seli, mazoezi, macho na
kichwa pia,” anasema Rehema.
Anasema lakini kila alipokwenda kufanyiwa tiba ya mazoezi
alipata maumivu makali mno ya mwili.
Alipofikisha umri wa miezi sita alianzishiwa dawa aina
ya ya hydroxyulea ambayo kwa kiasi kikubwa imemsaidia kupunguza maumivu ya
mwili yatokanayo na Siko Seli.
“Lakini changamoto sasa ikawa namna ya kumfikisha kliniki
zake, amekuwa sasa na ameongezeka uzito wa mwili wake.
Anasema japokuwa mwanawe anaishi na changamoto hizo
alizozaliwa nazo hakumficha ndani.
Shule alimpeleka kama watoto wengine wasio na changamoto
yoyote ile na amejaliwa pia mtoto mwingine wa kiume, hata hivyo baba yao sasa
ni marehemu.
“[Sabrina] sasa yupo darasa la saba, japo hajui kusoma wala kuandika lakini [nina furaha akienda shule, kwa sababu ] akiwa na wale
wenzake anafurahi [naamini kuna kitu anajifunza],” anasema.
MMETUPA
TABASAMU
Ukafika muda wa kukabidhi msaada wa kiti cha usaidizi
[wheelchair] kwa Sabrina, ambacho ni zawadi iliyonunuliwa na rafiki wa
mashujaa wa Siko Seli The Blood Drive
Network.
Taasisi hiyo yenye makao yake makuu nchini Nigeria
iliwasilisha msaada huo kwa Bone and Blood Foundation na Jumuiya ya Watu
wanaoishi na Siko Seli Tanzania ili kufikisha kwa familia hiyo.
Sabrina alipoketishwa katika kiti hicho, tulishuhudia
furaha yake, hasa pale alipokuwa akimtazama mama yake, alicheka kwa furaha
kubwa.
Kwa sababu ya changamoto aliyonayo ya mtindio wa ubongo Sabrina
hawezi kuzungumza kama watoto wengine isipokuwa kushirikisha hisia zake kwa
vitendo.
“Leo amefurahi mwanangu,” anasema Rehema huku naye
akifurahia msaada huo wa ‘wheelchair’.
“Nashukuru [taasisi hizi] wameniletea ‘wheelchair’
imenisaidia, wamekuja kututembelea
wameniletea zawdi hii itanisaidia mno.
“Kumpeleka shule, hata hospitali nilikuwa nikimbeba
mgongoni miguu inaning’inia chini, nikifika hospitali nitafute ‘wheelchair’
[wakati mwingine] pale nakosa,” anasema.
Anaongeza “[Basi inabidi] uzunguke naye [kupata huduma
mbalimbali ndani ya hospitali] huku unachoka.
“[Sasa] nitachukua bajaji itanipeleka mpaka Muhimbili au
kwa mwendokasi [wheelchair] itanisaidia mno.
MAUMIVU
YATAPUNGUA
“Hata marafiki zake pia watafurahia huwa wanakuja kumchekesha
na kumfurahia watakuwa wanamsukuma atafurahi,” anasema.
Rehema anabainisha “Hata mimi maumivu ya mgongo yatapungua,
nilikuwa napata shida ya kumbeba mgongoni,”.
Anasisitiza wazazi na walezi wenye watoto waliozaliwa na
changamoto mbalimbali kama mwanawe Sabrina wasiwafiche ndani.
“[Ukija hapa kwetu] watoto wote wanamjua, hata uulize mama
Sabrina anakaa wapi utaletwa.
“Wazazi [jamii] wanamfahamu,” anasema na kuongeza “Namshukuru
Mungu na nawashukuru madaktari wa Muhimbili tangu nimejifungua wanamuhudumia
kwa moyo mmoja.
“Bila wao ningemkosa ameumwa sana, tangu amezaliwa mpaka
leo anakunywa kidonge katika maisha yake.
“Dkt. Soka, Zamir, kombo, madaktari wa kitengo cha mazoezi,
macho wote nawashukuru sana,” anasisitiza Rehema.
TUMEFUNGUA
MILANGO
Mkurugenzi wa Bone and Blood Foundation Neema Mohamed
anasema imekuwa jambo la furaha kukabidhi msaada huo kwa familia ya Sabrina.
Anasema ni jambo jema kushirikiana kusaidia jamii, “Bone
and Blood Foundation, kazi yetu ni kutoa elimu ya msingi kuhusu Siko Seli [kwa
jamii].
“… pia kuhamasisha jamii kuchangia damu kwa hiyari ili
wagonjwa wanaohitaji ikiwamo wa Siko Seli wasikose huduma,” anasema.
Anafafanua kuhusu msaada waliokabidhi kwa Sabrina, “Tunaamini
kiti hiki kitamsaidia. Mtoto ana miaka 15 ameshakuwa mzito, inampelekea mama
yake kupata maumivu ya kifua [na mgongo].
“TBDN [The Blood Drive Network] wamekileta na sisi tumekabidhi
kitamsaidia Sabrina nyumbani na shule.
“Tumefungua milango yetu tunakaribisha taasisi zinazotamani
kufanya kazi na sisi [Bone and Blood Foundation pia Jumuiya ya Watu wanaoishi na
Siko Seli Tanzania] kusaidia watoto kama Sabrina,”.
Pamoja na hayo ametoa rai “Wazazi si vizuri kumficha mtoto
wako kumuweka mbali na huduma za afya, sasa zipo na zipo karibu nasi.
“Mpeleke apate huduma za msingi, tunaamini katika kila kitu
mzazi ukimpeleka hospitalini kupata huduma vile vile usiache kumpeleka shule
apate elimu,”.
Chapisha Maoni