moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema

Upo mkutano mkubwa wa kwanza wa kihistoria katika sekta ya afya unaokwenda kufanyika kwa siku mbili [Oktoba 29 na 30, 2024] ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

Ni mkutano wa 11 wa Merck Foundation ambapo hii ni taasisi kubwa duniani waanzilishi wake ni wa huko Ujerumani, makao yake makuu yakiwa Dubai.

Taasisi hiyo imejikita kwa miaka mingi kuangazia afya ya mwanamke, kupiga vita vitendo vya ukatili na unyanyapaa kwa waliokosa watoto pamoja na kuhimiza elimu kwa mtoto wa kike.

Hivi sasa ikizidi kutanua mbawa zake kuangazia pia masuala ya magonjwa yasiyoambukiza ikiwamo Kisukari na Shinikizo la damu.

Ni magonjwa yanayoathiri idadi kubwa ya watu hivi sasa ulimwenguni, Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa mkutano wa mwaka huu na hii ni hatua kubwa katika sekta ya afya.

Wageni kutoka nchi za Bara la Afrika na Asia wapatao 600 wanatarajiwa kuhudhuria mkutano huo wakiwamo wenza wa Marais kutoka nchi 15 za Afrika.

Kundi jingine ni la wataalamu wa afya hususan madaktari wakiwamo wale wa upandikizaji mimba.

Ujio huo unahusisha pia kundi la waandishi wa habari waliojikita sekta ya afya ambao ni mabalozi wa Taasisi hiyo kutoka nchi mbalimbali nao watashiriki.

KWANINI TANZANIA? 

Hili ni swali ambalo bila shaka unajiuliza, kwamba kwanini Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa mkutano huu mkubwa wa kimataifa kwa sekta ya afya. Makala haya yanakujuza kwa kina.

“Huu mkutano [ili ufanyike nchini husika, Merck Foundation] huwa mara nyingi wanangalia vingi,”. 

Yanaelezwa hayo na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mindi Kasiga.

Anaongeza “Kubwa [ni] jinsi nchi yako inavyokabiliana na changamoto mbalimbali aambazo zinaikumba jamii katika masuala ya afya na je umepiga hatua gani kuzitatua,”.

“Kwa hiyo tunakuja, kwa sababu ni kama kikao kazi [washiriki] wanaangalia zaidi wawekeze zaidi kwenye masuala yapi [kuboresha zaidi jitihada na huduma za afya kwa mataifa husika].

MFANO WA KUIGWA

Mtendaji Mkuu wa Merck Foundation Seneta Dkt. Rasha Kelej katika mkutano wake wa awali na waandishi wa habari uliofanyika Dar es Salaam hivi karibuni,

Anasema wameichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa mwaka huu kwani ni mfano mzuri wa kuigwa kutokana na namna ilivyofanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya.

Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi na ndiye ‘atakayebariki’ mkutano huo.

Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mama Maria Mwinyi  yeye atawakilisha upande wa Tanzania katika mkutano huo.

 “Washiriki wengine ni wataalamu na watafiti nguli katika sekta ya afya, wenza wa marais, watunga sera na waandishi wa habari,” anasema na kuongeza, 

"Tumeiteua Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huu kwani tumevutiwa mno na uwekezaji mkubwa uliofanywa  na Serikali katika sekta ya afya," anasema.

Dkt. Rasha anasisitiza “Uongozi wa Dkt. Samia ni mfano wa kuigwa, ndiyo maana hatujasita kuja Tanzania,”.

Ndani ya mkutano huo kutakuwa na makongamano yatakayoendelea ambapo wataalamu wote watajadiliana kwa pamoja na kupeana ujuzi na maarifa mapya.

Balozi Mindi anasisitiza “[Makongamano hayo] yanalenga kutoa elimu kwa madaktari, kwa hiyo kuna madaktari wa Tanzania wamejiandikisha tayari watashiriki.

“Wenza wa marais ndiyo wanaubeba huu mkutano, tayari wamewasili wengi nchini, walimuomba [Rais Samia mkutano huo uwe Tanzania] kwa sababu ya jitihada ambazo tumepiga.

“.., katika suala zima la afya na magonjwa ambayo yanaikabili jamii kwenye upande wa afya mama na mtoto,” anasisitiza na kuongeza.

“Kwa ile jihitada waliomba kwamba nchi yako ni mfano kwa hiyo tukifika tunaweza kupata nyenzo za kuwapa wenza wengine nini cha kufanya kwenye nchi zao.

“Rais alilidhia kwa sababu ni katika harakati za kujifunza na kuwafundisha wengine, wakija madaktari wako wakifundihwa inasaidia kutatu changamoto nyingine ambazo pengine siye hatujafikia.

Anaongeza “[Mada zilizochaguliwa kujadiliwa ni kuhusu] afya ya mama, ugonjwa wa saratani, ugonjwa wa kisukari na shinikizo la damu na mipango ya maendeleo ya kujengewa uwezo.

“.., wanaangalia Tanzania mmefikia wapi na tuweke nguvu katika maeneo gani. Tunatazamia watu 600 kutoka nje wanakuja Tanzania kwa ajili ya kushiriki mkutano huo,”.

Anasema pia kuna Watanzania waliojiandikisha hivyo idadi hiyo itaongezeka na kwamba kuna watu kati ya 400 na 500 ambao watadhuhuria kwa njia ya mtandao.

USHIRIKIANO MADHUBUTI

Kwa miaka miaka mingi Merck Foundation imekuwa ikishirikiana bega kwa bega na Tanzania hasa katika kufadhili masomo kwa wataalamu wa sekta ya afya.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima anasema,

“Mawaziri wa afya, jinsia, mawasiliano, elimu, ustawi wa jamii kutoka nchi zilizoalikwa watashiriki mkutano huu,”.

Anasema mkutano huo utafungua njia ya utekelezaji wa ahadi mpya zitakazotolewa na wenza wa marais, mawaziri na timu ya Merck Foundation.

"Ni katika kuhakikisha upatikanaji wa suluhu bora na usawa wa huduma za afya na watu wa Afrika hasa kutoka nchi zitakazokuwepo katika mkutano huu, ikiwamo Tanzania.

Anasema utatumika kama jukwaa la kuchukua hatua mahususi katika kushughulikia unyanyapaa na mtazamo wa kijamii wa utasa.

"Kuboresha upatikanaji wa huduma za uzazi salama iliyodhibitiwa na yenye ufanisi kwa wanawake na wasichana," anabainisha Waziri Gwajima.

Anasema washiriki watanufaika na maarifa na uzoefu unaotolewa na wataalamu mbalimbali na watafiti ambao watazungumza kwa kina mada zitakazowasilishwa.

“Nchi zingine ambazo mkutano wa namna hiyo umefanyika kwa awamu zilizopita ni pamoja na Ujerumani, Kenya, Cote d'Ivoire, Misri na Mauritius.

“Mkutano huo pia umekwisha fanyika katika nchi za Senegal, Ghana, Zambia, Umoja wa Falme za Kiarabu pamoja na India,” anabainisha.

SEKTA YA UCHUMI

Balozi Mindi anabainisha mikutano mikubwa kama huo husaidia kuchochea uchumi na kuongeza fedha za kigeni ikiwamo Dola.

“Kwa mfano [ikiwa mtu mmoja atatumia kiasi cha] Dola 1000 [ukipiga hesabu kwa washiriki] 600 [maana yake ni wastani wa] Dola 600,000 [watatumia].

“[Hii ni sawa na kiasi cha] Tsh. Bil. 1au 2 na hiyo ni makisio ya [matumizi kwa] ‘minmum’ [lakini ikiwa mtu] ataamua ku-spend zaidi ya hapo,

Anaongeza “…, nadhani kwa wakati mmoja itachechemua uchumi wetu na watu wadogo wadogo eneo la Dar es Salaam ambako [mkutano] utafanyika.

SEKTA YA HABARI

Siku ya pili ya mkutano huo ni mahususi pia kwa kundi la waandishi wa habari ambapo watakuwa na semina maalum ya kuwajengea uwezo wa umahiri katika habari za afya.

“Wametoa kipaumbele kutoa mafunzo maalum kwa waandishi wa habari ambao wamejikita kwenye kuandika habari za afya,” anasisitiza Balozi Minde.

Anaongeza “[Merck Foundation] wanasema kama mwandishi wa habari hajajua vizuri jinsi ya kuandika, kwa mfano magonjwa sugu, uzazi.

“Mwandishi ajue jinsi ya kuiandikia, Tanzania wametoa fursa waandishi kujiunga [kushiriki],”.

Anasema hii ni tofauti kabisa na mikutano na makongamano mengine ambapo kundi hili hufika tu kuripoti habari na kuondoka.

Anasema hatua ya kuwapo kwa semina hiyo kwa waandishi itawajengea uwezo zaidi kuboresha maudhui ya afya popote watakapokwenda kukusanya taarifa zao ili kusaidia jamii na Taifa.

KISWAHILI/TEKNOLOJIA Ai

Ai hii ni miongoni mwa mada ambazo kwa mwaka huu pia itawasilishwa katika semina hiyo kwa waandishi wa habari.

"Ni eneo mojawapo ambalo tumeliangalia na kuona linafaa kwa waandishi kupatiwa mafunzo maalum," anasema Seneta Rasha.

Anabainisha Merck Foundation pia kuanzia sasa itaanza kujumuisha lugha adhimu ya kiswahili katika nyenzo zake za kupeleka ujumbe wa afya kwa jamii ya Watanzania.

Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa Taasisi hiyo kutumia lugha ya kiswahili ambapo awali imekuwa ikitumia lugha nyinginezo ikiwamo kingereza na kifaransa.

"Mimi mwenyewe pia nimeanza kujifunza maneno ya kiswahili, kwa mfano najua kutamka neno saratani hii inamaanisha cancer kwa lugha ya kingereza," anasema.

UTALII TIBA/MIKUTANO

Hili ni eneo jingine ambalo Tanzania itanufaika nalo, utalii wa matibabu na utalii wa mikutano ambapo haya ni mazao mapya ya utalii.

“Tuendelee kuvutia, kwa sababu wanapokuja madaktari wakiona kwamba tuna uwezo tumeendelea basi mkutano mwingine wa madaktari wa taasisi nyingine wanaweza pia wakachagua.

Anasisitiza hayo Balozi Mindi na kuongeza, “.., Tanzania [Dar es Salaam] kwa sababu ya ukaribu wake na Zanzibar.

"Lakini pia wataona tuna maeneo mengine mbalimbali ya kuwawezesha kufanya malazi ya hawa washiriki wa mkutano.

“Ambapo kwa nchi nyingine wanakuwa wanakwama kwenye maeneo hayo,” anabainisha.

Anatoa rai kwa balozi za Tanzania katika nchi mbalimbali kuendelea kuvutia taasisi na mashirika ili zije nchini kufanya mikutano kama hiyo kama ulivyofanya Balozi wa Falme za Kiarabu.

“Balozi [wa Tanzania katika Falme za Kiarabu] ameshiriki kwa kiasi kikubwa [kuhimiza ujio wa mkutano huo] kwa sababu ni mojawapo ya maeneo ambayo tunayapigia chapuo katika balozi zetu.

Anaongeza “Ukienda huko nchi tunaangalia jinsi ya kuvutia mikutano hii ya kimataifa,

“Tuendelee kushirikiana kuvutia uwekezaji, utalii wa mikutano pia kama sekta binafsi tuendelee kushirikiana bega kwa bega kuhimiza waandaaji waweze kuja Tanzania,” anatoa rai.

JAMII KWA UJUMLA

Balozi Mindi anasema mkutano huo ni wenye tija kwa Taifa kwani madaktari watapata ujuzi na maarifa mapya ambapo watakaporejea kwenye vituo vyao vya kazi watayatumia kuboresha huduma.

“Elimu watakayopata watakwenda kuongeza jitihada kwenye eneo la kazi,” anasisitiza.

Anasema tayari Wenza wa Marais 15 wameshawasili na kila mmoja amefika na wajumbe wake.

“Waziri wake wa afya au maendeleo ya jamii, elimu au mawasiliano inategemea [jinsi] wizara zao zimejipangaje,” anabainisha.

Anasema pamoja na hayo, baada ya muda fulani Tanzania itafanya tathmini ya kina kuangalia namna ilivyonufaika kwa ujumla kwa mkutano huo utakaofanyika kwa siku hizo mbili.

Baadhi ya nchi ambazo wenza wa marais wake wanashiriki ni pamoja na Botwasana Burundi, Zambia, Zimbabwe, Ghana Kenya, Sao Tome, Cape Verde, Afrika ya Kati na Mwenyeji Tanzania.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement