Na Mwandishi Maalum
Kila siku, Rahma
Abdallah hulazimika kufikiria jambo moja muhimu kabla ya mambo mengine ‘dawa
yake’.
Anaishi Chanika, Dar
es Salaam, Rahma ni mmoja wa watu wanaoishi na Ugonjwa wa Siko Seli ambao
hutegemea dawa ya hydroxyurea kusaidia kudhibiti athari za ugonjwa huo.
Kwa siku, yeye anatumia
vidonge viwili vya dawa hiyo, ambapo kila kidonge hununua kwa Sh2,000.
“Ni changamoto sana,
hasa unapokuwa huna kazi na unategemea ndugu,” anasema.
Kwa wagonjwa wengi wa
Siko Seli, hydroxyurea si dawa ya kawaida tu.
Inaweza kuwa sehemu
muhimu ya maisha yao, hususan katika kusaidia kupunguza baadhi ya madhara na
vipindi vya maumivu makali vinavyoweza kujirudia.
Ndiyo maana taarifa za
Senegal kuanza uzalishaji wa dawa hiyo zimepokelewa kwa matumaini mapya
miongoni mwa baadhi ya watu wanaoishi na ugonjwa wa Siko Seli na wadau wa afya Barani
Afrika.
Rahma anaona hatua
hiyo kama jambo la kujivunia kwa Bara la Afrika.
“Senegal kuanza
utengenezaji ni hatua nzuri, kwa sababu bei ya dawa inaweza ikazidi kupungua
ili tuzipate kwa wingi,” anasema.
Hatua ya matumaini
kwa Afrika
Daktari Collin Kanza
kutoka Sickle Cell Center - Muhimbili anaelezea hatua ya Senegal kama mafanikio
makubwa kwa mapambano dhidi ya Siko Seli Barani Afrika.
“Ni hatua kubwa sana.
Senegal ina wagonjwa wachache wa Siko Seli ikilinganishwa na baadhi ya nchi
nyingine za Afrika lakini imeweza kufanya jambo hili kubwa.
“Sisi tuna uhitaji
mkubwa zaidi wa dawa hizi. Ni wazi tunalo la kujifunza na kuiga mfano kutoka
kwao,” anasema.
Tanzania inashika
nafasi ya nne duniani na ya tatu Barani Afrika kwa nchi zenye idadi kubwa ya
wagonjwa wa Siko Seli, kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO).
Takwimu za Wizara ya
Afya zinaeleza kila mwaka kuna Watoto 11,000 hadi 14,000 wanaozaliwa na ugonjwa
huo kila mwaka nchini Tanzania.
Matibabu dhidi ya
ugonjwa huu wa kurithi ni ya muda mrefu, uwezo wa dawa muhimu kupatikana kwa
urahisi na kwa gharama nafuu unaweza kuleta tofauti kubwa katika maisha ya
wagonjwa na familia zao.
Hatua ya Senegal pia
inafungua mjadala mpana kuhusu uwezo wa Afrika kuwekeza katika uzalishaji wa
dawa muhimu zinazohitajika na watu wake.
Kwa sasa, baadhi ya
dawa zinazotumiwa na wagonjwa wa Siko Seli Tanzania zinaendelea kupatikana
kupitia uzalishaji na mifumo ya usambazaji kutoka nje ya Bara la Afrika,
ikiwamo hii ya hydroxyurea.
Iwapo uzalishaji wa
hydroxyurea utaongezeka Barani Afrika na dawa hiyo kusambazwa katika nchi
nyingine, matumaini ya wagonjwa wengi ni kwamba gharama inaweza kushuka na
upatikanaji wake kuongezeka.
Bima ya afya
inapunguza mzigo
Wizara ya Afya
Tanzania iliingiza dawa hii katika orodha ya dawa zinazopatikana ndani ya bima
ya afya.
Kwa Felister John,
mzazi wa shujaa wa Siko Seli anayeishi Kigoma, kuwa na bima ya afya kwa mtoto
wake kumeleta mabadiliko makubwa.
Anasema kabla ya
kuweza kumkatia mtoto wake bima ya afya, familia yake ilipitia changamoto kubwa
kwa sababu alilazimika kutoa fedha kutoka mfukoni kununua dawa na kugharamia
huduma za matibabu.
“Lakini baada ya
kupata bima, hali imeanza kubadilika. Kwa sasa, anaweza kumudu baadhi ya
gharama za matibabu ya mtoto wake kupitia bima ya afya,” anasema.
Hata hivyo, kwa
familia ambazo hazina uwezo wa kugharamia bima, mzigo wa Siko Seli unaweza kuwa
mkubwa zaidi.
Julieth Mombuli ni
miongoni mwa wale wanaopambana kila siku kuhakikisha mtoto wake anapata dawa.
“Nashindwa. Mimi ndiye
baba na mimi ndiye mama, baba yake alikataa kwamba huyu sim toto wake,
nimempata na mwanaume mwingine nje ya ndoa, jambo ambalo si kweli.
“Hivyo, sina jinsi ya
kufanya. Naumia, lakini ni mwanangu siwezi kumuacha akiteseka peke yake,
ninafanya biashara ndogondogo, kuna wakati nalazimika kujinyima ili angalau
mwanangu apate dawa,”.
Anasema mwanawe
anapotumia dawa yahydroxyurea huwa na nafuu kubwa, humsaidia kupunguza vipindi
vya maumivu makali vinavyojirudia mara kwa mara.
Kwa Julieth, kutafuta
fedha za dawa ni sehemu ya mapambano ya kila siku ya kumlea mtoto anayeishi na
Siko Seli.
Mahitaji ni makubwa
Veronica Mrema, Afisa
Habari wa Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Siko Seli Tanzania (SCDPCT), anasema
jumuiya hiyo imekuwa ikisaidia baadhi ya watoto wanaoishi na ugonjwa huo kupata
bima ya afya.
“Lakini mahitaji bado
ni makubwa. Kwa mfano tangu Januari
mwaka huu hadi sasa, tumeweza kuwakatia bima ya afya watoto 36 tu kwa
kushirikiana na mdau mmoja aliyetuunga mkono.
“Orodha tuliyonayo
bado tuna wengine wengi ambao hatujaweza kuwafikia kwa sababu uhitaji ni
mkubwa,” anasema.
Veronica anasema
juhudi hizo hutegemea kwa kiasi kikubwa msaada kutoka kwa wadau mbalimbali.
“Tunaweza kuwasaidia
pale tunapopata wadau wanaotuchangia na kutuwezesha kuwakati bima za afya. Kuna
wadau pia hutusaidia kununua dawa hizi na sisi huzigawa bila malipo kwa baadhi
ya mashujaa wenye uhitaji.”
Anasema, kwa muktadha
huo, hatua ya Senegal kuanza uzalishaji wa hydroxyurea ni hatua inayostahili
pongezi kubwa na ina maana kubwa katika mapambano dhidi ya Siko Seli.
“Kwa hatua ambayo
Senegal imeweza kufikia, imetuletea faraja kubwa. Ni hatua kubwa, na mashujaa,
wazazi na walezi wameipokea kwa furaha kubwa,” anasema.
Je, bei itashuka?
Kwa wagonjwa
wanaonunua dawa kila siku, swali kubwa sasa ni iwapo uzalishaji wa hydroxyurea
ndani ya Afrika utaweza hatimaye kushusha gharama zake.
Watu wanaoishi na Siko
Seli Tanzania wana matumaini kwamba iwapo Senegal itafikia uwezo wa kuzalisha
dawa kwa kiwango cha kutosheleza na kuisambaza katika nchi nyingine za Afrika,
ikiwamo Tanzania, gharama za ununuzi zinaweza kupungua kwa kiasi kikubwa.
Kwa Rahma, ambaye kwa
sasa hununua vidonge viwili kwa siku, matumaini hayo yana maana kubwa.
Uzalishaji wa dawa
ndani ya Afrika unaweza kuwa mwanzo wa safari ndefu kuelekea upatikanaji wa
dawa kwa gharama nafuu zaidi kwa wagonjwa wengi.
Hatua ya Senegal, kwa
hiyo, si habari ya kiwanda pekee. Kwa wagonjwa wa Siko Seli kama Rahma, wazazi
kama Felister na Julieth, na mashirika yanayopambana kusaidia wagonjwa nchini
Tanzania.
“Ni ishara ya
matumaini kwamba siku moja dawa muhimu kwa maisha yao zinaweza kupatikana kwa
urahisi zaidi na kwa gharama ambayo familia nyingi zinaweza kuimudu,” anasema
Veronica.
Kwa Afrika, huenda huu ukawa ni mwanzo wa kujenga uwezo wa kuzalisha zaidi dawa zinazohitajika na watu wake badala ya kuendelea kutegemea matumaini yanayotoka mbali.

Chapisha Maoni